WAZIRI WA ELIMU ATEMBELEA ENEO LA UJENZI WA KAMPASI YA UDOM NJOMBE


  • 10 hours
  • The University of Dodoma

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda ( Mb) tarehe 20 Septemba, 2024 ametembelea eneo la ujenzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma Kampasi ya Njombe lililopo Halmashauri ya mji wa Njombe katika ziara yake ya kutembelea na kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita Mkoani Njombe.

Prof. Mkenda amefurahishwa na hatua liyofikiwa na UDOM ya hatua za awali za ujenzi wa kampasi ya UDOM mkoani hapo katika utekelezaji wa Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi ( HEET) ambayo itakuwa Taasisi ya Kwanza ya Elimu ya Juu katika mkoa huo.

"Lile ombi la wananjombe walilolitoa kupitia viongozi waliochaguliwa na wananjombe limekamilika fedha zimetengwa ukandarasi shughuli zinakwenda tunatarajia 2026 hapa tutaanza kuona wanafunzi wanakuja " Alisisitiza Prof. Mkenda.

Naye; Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma, Utafiti na Ushauri Elekezi Prof. Razack Lokina amesema ujenzi wa Kampasi hiyo utaanza Disemba 2024, utagharimu shilingi bilioni 20 na ujenzi ukikamilika chuo kinatarajiwa kuchukua wanafunzi 1000 na kitaanza kwa kutoa programu za stashahada na shahada za ujuzi katika fani za kilimo, TEHAMA, Misitu pamoja na mazao yake na zingine zinazoendana na shughuli za kiuchumi za Mkoa wa Njombe.

Kwa upande wa Mbunge wa Njombe Mjini Mhe. Deo Mwanyika amewataka wakazi wa Njombe kutumia fursa ya ujenzi wa chuo hicho kupata elimu lakini kuinuka Kiuchumi kutokana na ujio wa wageni chuo hapo.

Comments
Send a Comment