TAASISI YA UDOPRESA YAZINDULIWA UDOM
Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko Chuo Kikuu cha Dodoma, Bi. Rose Joseph leo Jumamosi tarehe 24 Mei 2025, katika Ukumbi wa LT2 (CHSS) UDOM amefanya Uzinduzi wa Taasisi ya Wanafunzi wanaosomea Uandishi wa Habari na Uhusiano wa Umma Chuo Kikuu cha Dodoma - The University of Dodoma Public Relations Students Association (UDOPRESA) yenye jumla ya wanachama 250.
Taasisi hiyo imeanzishwa kwa dhamira kuu ya kuwaunganisha wanafunzi wanaosoma Taaluma ya Uhusiano na Umma na Uandishi wa Habari wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Kuimarisha Taaluma, Kushirikiana katika Tafiti na Mafunzo na kuwa chachu ya Maendeleo ya Taaluma hiyo Nchini.
Akizungumza wakati wa Hafla ya Uzinduzi; Mkurugenzi wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko Chuo Kikuu cha Dodoma Bi. Rose Joseph ameahidi kuwapa ushirikiano wowote watakaohitaji huku akiwaasa kutumia Taasisi hiyo katika kulinda taswira ya Chuo na kuwataka watangulize uzalendo kwa Taifa mbele, kulinda na kuheshimu fani hiyo; pamoja na kuzingatia Sheria, Taratibu na Miongozo yote ya maafisa Uhusiano na Habari.
"Hili ni Jukwaa muhimu sana ambalo si tu kwamba linawaleta pamoja wanafunzi wanaosomea Uhusiano wa Umma UDOM, lakini naamini ni jukwaa zuri la kuwanoa, kuwaweka tayari kwa ajili ya kwenda kulitumikia Taifa, kutetea Tasnia na kwenda kuwa waandishi bora na maafisa bora wa umma" Aliongeza Bi. Rose.
Kwa Upande wake; Mkuu wa Idara ya Sanaa na Taaluma za Habari, Dkt. Deograsia Ndunguru amewapongeza Wanachama wote wa UDOPRESA huku akisisitiza kuwa Taasisi hiyo itawasaidia kuongeza ujuzi, Maarifa hasa katika kuwajenga kuwa maafisa Uhusiano Bora wa baadae.
Naye; Mlezi wa Taasisi hiyo Dkt. Mary Kafyome, amesema ulikuwa ni mchakato mkubwa kufanikisha jambo hilo huku akitoa pongezi kwa wote walihusika kufanikisha tukio hilo na ametoa wito kwa wanafunzi wanaobaki kuendeleza taasisi hiyo.
"UHUSIANO BORA, JAMII BORA!"