KUSILUKA AWATAKA WATAALAMU WA MAZINGIRA UDOM KUREJESHA UOTO WA ASILI DODOMA.


  • 2 weeks
  • The University of Dodoma
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dodoma Prof. Lughano Kusiluka amewataka wataalamu wa Mazingira UDOM kutumia taaluma yao kurejesha uoto wa asili wa Dodoma uliopotea kutokana na shughuli mbalimbali za kibinadamu.
 
Rai hiyo ameitoa katika mdahalo ulioandaliwa na Idara ya Jiografia na Stadi za Mazingira UDOM uliofanyika tarehe 4/6/2024  wenye kauli mbiu “Urejeshwaji wa Ardhi na Ustahimilivu wa Hali ya Jangwa na Ukame” uliohusisha wadau wa mazingira kutoka ndani na nje ya UDOM.
 
" Tuna wanasayansi, walimu na  wahandisi wa Mazingira lakini tuna watalaamu wa kuzuia majanga, UDOM tukiwa kama wasomi ambao sauti zetu zinasikika mbali  tunatakiwa tusaidie jamii inayotuzunguka kutunza na kuhifadhi mazingira hasa sehemu zote zenye makorongo hapa Dodoma
" Aliongeza Prof. Kusiluka.
 
Aidha, Prof. Kusiluka amewapongeza  wana jumuiya wa Chuo Kikuu cha Dodoma kwa kuendesha kampeni mbalimbali  za utunzaji na uhifadhi wa Mazingira ndani ya Chuo ikiwemo kampeni ya kijanisha UDOM.
 
Mtoa mada kutoka Idara ya Jiografia na Stadi za Mazingira UDOM Prof. Abiud Kaswamila  ambaye aliwasilisha mada juu ya Binadamu; Dunia inahitaji kuponywa sio kuumizwa alitaja mambo makuu 3 ambayo yanasababisha uharibifu wa mazingira kuwa ni ongezeko la watu, umaskini na mabadiliko ya hali ya hewa. 
 
Muwasilianaji mada kutoka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira ( NEMC)  Bwn. Emmanuel Mwasihu amesema kama NEMC wanaendelea kutoa  Elimu kuhusu utunzaji na uhifadhi wa Mazingira  na  amependekeza kuwa mitaala katika ngazi zote za elimu izingatie elimu ya mazingira.
 
Naye, Mwanafunzi wa Mwaka wa tatu wa Shahada ya Awali ya Sanaa katika Giografia na Sayansi ya  Mazingira kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma Bi. Mariam Philip amesema yeye atakuwa balozi mzuri wa mazingira na ataitumia vizuri mafunzo aliyopata katika kubadilisha jamii inayomzunguka. 
 
Chuo Kikuu cha Dodoma kimeahiriki katika shughuli mbalimbali za uifadhi wa Mazingira kuanzia tarehe 1/6/2024 ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa umma na kufanya usafi maeneo mbalimbali ya jiji la Dodoma. UDOM pia itashiriki katika kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani tarehe 5 Juni, 2024 ambayo kitaifa yatafanyika jijini Dodoma katika Ukumbi wa Jakaya Kikwete.
 
 
 
 
 
Comments
Send a Comment